Tuesday, 6 February 2024

MSAMAHA NA DHANA ZAKE


 

 

Ndugu wasomaji karibuni katika Makala yetu ya leo ambayo inahusu jambo muhimu na msingi wa uwepo wa amani na utulivu katika maisha yetu ya kila siku. Mada hii ya msamaha ni muhimu kwa sababu inahusisha hisia za mtu moja kwa moja katika kufanya maamuzi baada ya kukosewa au kukosea.

Neno Msamaha linatafsiriwa kwa dhana mbalimbali kama ni uamuzi wa Mwenyezi Mungu au mtu mwingine wa kuamua kutofuatilia matendo na makosa ambayo ametendewa na mtu mwingine.

Katika Luka 6:37 imeelezwa kuwa maana ya msamaha ni "kuachilia". achilieni nanyi mtaachiliwa.

Katika Quraani Surat taghabun aya ya 14 imeeleza maana ya neno msamaha na hatua zake ambapo imefafanuliwa kuwa msamaha au kuwia radhi ni hali ya kutotilia mkazo au maanani kosa lililofanyika hii kwa mujibu wa Imamu Ali (A). Msamaha ni taji la sifa kwa muungwana. Pia katika aya hii imeeleza kuwa msamaha ni uvumilivu ambao unazuia kuadhibu kwa maneno au vitendo, kadhalika msamaha ni kufuta kile kitendo kilichofanywa na kuondoa dhana ya matokeo hasi ambayo yametokana na kufanyiwa makosa.

Vile vile tafsiri hii ya neno kabisa cha neno kisasi kupatana na aliyekiri msamaha inazidi kueleza kuwa ni kinyume lakini ni tofauti na neno kusahau, kutetea au makosa. Hii ina maana kuwa mtu anaweza akakusamehe ila bado akawa hajasahau lile jambo au tukio alilotendewa na mtu aliyemkosea.

Kwa upande wa dini zote unasisitiza na kuhimiza watu kusamehe pindi wanapokosewa, hali hiyo ya kusamehe inaleta nguvu hasa kwa mtu anayetoa msamaha na nafuu hiyo inaweza kuenea kuanzia katika nafsi ya mtoaji msamaha hadi mwilini kwake kote.

Msamaha siku zote unajumuisha mambo matatu ambayo ni msamaha wenyewe, uvumilivu na kuachiliwa.

Chanzo kikuu cha msamaha kilianza pale dhambi na makosa yalipoanza maana pasipo na dhambi na makosa msamaha usingekuwepo. Hivyo msamaha upo maalumu kwa ajili ya wale binadamu ambao ni watenda dhambi na wafanya makosa.

Kwahiyo, tambua kwenye dhambi na makosa hapo ndipo penye msamaha. Kuomba msamaha ni roho na mtu ambaye atagoma kuomba msamaha basi huyo ana roho ya kishetani maana naye aligoma kuomba msamaha pindi alipomkosea Mwenyezi Mungu na Shetani kuahidi kuwa atawapoteza na waja wengine.

Ili uwe mtu mwenye uwezo wa kutoa msamaha dhidi ya aliyekukosea lazima uwe na sifa zifuatazo.

Uwe mtu mwenye huruma, mtu mwenye uvumilivu, mtu mwenye upendo dhidi ya wengine, lazima uwe mtu uliye na hofu ya Mwenyezi Mungu pamoja na kumjua Mwenyezi Mungu na kwamba Mungu yeye ndiye aliyeanzisha msamaha kwa wanaomkosea mwisho mtu mwenye uwezo wa kutoa msamaha huwa ambaye anajua umuhimu wa msamaha pindi anapokosewa.

Je, utatambuaje au dalili na ishara za mtu aliyekusamehe baada ya kumkosea.

Hawezi kukuzungumzia vibaya mbele ya watu wengine, atakuchangamkia tena kama ilivyokuwa kabla ya kukoseana, endapo utapatwa au utakuwa na shida au tatizo hatosita kukusaidia na atakusaidia bila kinyongo chochote, pia mtu aliyekusamehe atakuwa anakusalimia na kupokea salamu zako pindi unapomsalimia kama ilivyokuwa zamani.

Vile vile katika tendo zima la msamaha mtu anayekusamehe anaweza kufanya hivyo bila kumuomba msamaha ila kama itatakiwa aliyekosea mpaka aombe msamaha yeye kuna mambo muhimu ya kuzingatia ambayo ni:-

Afahamu na kujua njia sahihi ya kuomba msamaha ikiwa hata kulia au kupiga magoti ili amridhishe anayemuomba msamaha, mwombaji msamaha afahamu umuhimu wa kuomba msamaha juu ya lile kosa alilotenda, ajue njia sahihi na namna ya kuacha kutorudia kosa alilotenda awali, mwisho na kwa umuhimu awe na imani kuwa Mwenyezi Mungu amehimiza kuomba msamaha pale tunapokoseana.

Wito wangu ni kuwa makosa kwa maumbile ya mwanadamu ni jambo la kawaida ingawa anaweza kukosea bahati mbaya ama makusudi. Hata hivyo kwa hali yoyote ile bado haizuii kwa mtu aliyekosea kusamehewa kwa kosa alilotenda. Siku zote msamaha huleta furaha na amani ya moyo hii itasaidia kupata jamii na Taifa lenye upendo, utulivu na amani ambapo itasukuma uwepo wa maendeleo kwa vizazi husika.

Friday, 2 February 2024

UISLAMU UNAHIMIZA MAADILI MEMA NA KUWATENDEA MEMA WANAADAMU WOTE HATAWASIO WAISLAMU



MWENYEZI Mungu (S.W) amemtuma Mtume wake Muhammad (S.A.W.) kwa ajili ya rehma kwa walimwengu wote, ambapo Mwenyezi Mungu (S.W) amesema "Nasi hatukukutuma ila uwe ni Rehema kwa walimwengu wote" Surat Al - Anbiyaa, aya 107 aya hii inatufundisha kuwa ujio wa Mtume Muhammad (SAW) ni rehema ya Mungu kwa viumbe wote waislamu na wasio waislamu, waarabu na wasio waarabu kwani mafundisho yake yangefuatishwa duni ingekuwa mahala pa amani.

Mafundisho ya dini ya kiislam yanawataka Waislam wawe na huruma kwa binaadamu wote waliopo duniani, Mtume Muhammad (S.A.W) amesisitiza maana hiyo kwa kusema "Hakika Mwenyezi Mungu hawahurumii wasiowahurumia wanandamu wenzao"hadithi hii ya mtume haikusema waislamu wenzo pekee bali imeongelea binaadamu kwa jumla.

Hivyo, Wanadamu wote wanatakiwa kuhurumiana bila kujali itikadi ya dini zao, kabila wala rangi, ambapo moja wapo ya misingi ya tabia njema katika dini ya kiislamu ni kuwaonea huruma wasio Waislamu na kuwatendea wema muda wakua hawajawafanyia uadui waislamu ama vitendo viovu.

Tukizisoma aya za Qur.ni ama kufuatilia hadithi za Mtume Muhammad (SAW) TUTATAMBU KUWA, huruma katika Uislamu ni jambo la viumbe wote, siyo kwa watu maalumu wala kwa baadhi ya Viumbe tu. Mtume Muhammad (S.A.W) amesema; "Kwa kweli Mwenyezi Mungu hamuhurumii ila aliye wahurumia wengine, Maswahaba wakasema; Ewe Mtume! Sote hivyo kwa maana tunawahurumia wengine. Mtume akasema, sikusudii mnavyofanya na wenzenu, bali na wanadamu wote".

Hivyo, alama ya kwanza ya kupambika na tabia nzuri katika mfumo wa maadili mema ya kiislam ni kuwahurumia viumbe wote hadi wanyama na si binadamu peke yao tunajifunza hilo katika mafundisho mema ya dini ya kiislamu.

Mtume Muhammad (S.A.W) amesema kuwa "aliadhibiwa mwanamke kwa ajili ya kumtesa Paka aliyemfungia ndani hakumpa chakula wala hakumuachia ajitafutie mwenyewe chakula, jambo hilo likasababisha aingie motoni". Katika hadithi hii tunajifunza jinsi huruma ilivyokuwa muhimu kwa mujibu wa mafundisho ya dini tukufu ya kiislam.

Mtume alikuwa ni mfano bora wa huruma kwa viumbe wote hata wanyama, katika maelekezo kwa umma huu anasema ( Hakika Allah ameagiza kufanya wema katika kila kitu hivyo hata mkichinja wanyama kwa ajili ya chakula wachinjeni vizuri ) na katika hadihi nyengine anasema ( mmoja wenu akimchinja mnyama anoe kisu chake vizuri na amlaze vizuri mnyama anayemchinja ili afanye jambo hilo kwa haraka).

Hadithi iliyotangulia inaelekeza huruma hata katika vitu vya machungu, sote tunajua kuwa, ng'mbe, mbuzi, kuku na wanyama wengine wanaoliwa kitendo cha kuwachinja ni kitendo cha maimivu kinacho sitisha uhai wao ili watumiwe kuwa ni kitoweo, hata hivyo bado Mtume anahimiza kuwa zoezi hilo lifanywe kwa huruma kisu kinolewe vizuri ili mnyama asiwe kwenye maumivu muda mrefu,

Mfano mwingine ni maelekezo aliyoyatoa mtume Muhammad kuhusu kukataza kuwatukana wafuasi wa dini nyengine wanaoishi katika miji ya waoslamu kwa makubaliano, pale aliposema "atakemtukana mfuasi wa dini nyengine anaekaa katika miji ya kiislamu kwa makubaliano ya Amani (dhimmyyu) zitampata laana za Mwenyezimungu" maelekezo haya yanahimiza kuwatendea maadili mema watu wa Imani nyengine.

Tukiangalia dhana iliyojengeka na baadhi ya wanaharakati wa kiislamu nchini Tanzania ni kuwa asiye muislamu hana haki ya kuishi, kuheshimiwa ama kuhurumiwa uelewa huu ni kinyume na mafundisho ya dini ya kiislamu, kwani rejea zote hapo juu zinaeleza kuwa waislamu wanatakiwa kukaa kwa wema na watu wote bila kujali dini zao na itikadi zao.

Kwa nchi kama Tanzania ambapo kuna idadi inayokaribiana ya waumini wa dini mbili mafunzo haya ya dini ya kiislamu ni wajibu kutekelezwa kutoka pande zote ili jamii ya watanzania iendelee kuishi kwa utulivu na Amani ili kujenga jamii salama inayopendana, hii itasaidia kuto wapa nafasi baadhi ya watu wenye nia ya kuwagombanisha watanzania kwa kigezo cha dini.

Ni matarajio yangu kuwa, kila muislamu nchini Tanzania na kwengine duniani atakae soma Makala hii atakuwa na huruma kwa waislamu wenzake na jamii yake bila kujali Imani na itikadi ya jamii hiyo ili awe ni kioo kwa jamii inayomzunguka tukiishi hivi maovu na uhalifu katika jamii utaisha na kufanya jamii iishi kwenye upendo na maelewano.



 

Monday, 29 January 2024

KWA NINI IBADA HAZITUBADILISHI TABIA ZETU?


 

 TUJIULIZE, KWA NINI IBADA HAZITUBADILISHI TABIA ZETU?


IBADA ni msamiati unaojumuisha utii kwa Mola wetu Muumba. Maana ya utii huu ni kufuata maamrisho ya Mola wetu Muumba na kuacha makatazo yake.

Ibada kwa tafsiri ya kutenda maamrisho na kuacha makatazo ya Mola wetu Muumba huwa zinambadilisha yule anayeabudu. Mtu anayefanya ibada huwa anabadilika kutokea kwenye tabia mbaya na kuwa na tabia nzuri zinazopendwa na kupendeza katika jamii.

Mwenyezi Mungu anasema katika Sura ya 29 (Al-Ankabuut) Aya ya 45: "Na simamisha Swala, hakika Swala inakataza machafu na madhambi."

Aya hiyo inaonyesha kwamba anayeswali atakatazika na machafu na maovu mengine kutokana na ile nguvu ya swala.

Katika ibada ya saumu, Mwenyezi Mungu anasema katika Sura ya 2 (Al- Baqarah) Aya ya 183: "Enyi Waumini mmefaradhishiwa kufunga kama walivyofaradhishwa (kufunga) waliokuwa kabla yenu ili mpate kuwa wacha-Mungu."

Aya hiyo inaonesha kwamba anayefunga atakuwa mcha-Mungu kwa mana ya kuwa na tabia ya kujikinga na madhambi.

Katika ibada ya Zaka, Bwana Mtume Muhammad (Swallallaahu Alayhi Wasallam) anasema: "Zijengeeni ngome mali zenu kwa kutoa Zaka." Hadithi hiyo inabainisha kwamba anayetoa Zaka pamoja na faida aliyoipata kwa kusimamisha ibada, lakini pia ameijengea ulinzi mali yake haitopatwa na madhara, maangamivu wala hilaki yoyote.

Katika ibada ya Hijja, Bwana Mtume Muhammad (S. A. W.) anasema: "Yeyote mwenye kuhiji na asiseme maneno machafu na asifanye madhambi, atatoka katika madhambi yake (atasamehewa) kama siku aliyozaliwa (alivyokuwa hana dhambi)."

Hadithi hiyo inaonyesha kwamba ili ibada ya Hijja ikubaliwe lazima anayehiji awe na tabia njema na tabia njema ni jambo endelevu linalotakiwa kuwapo kwa muumini. Hivyo, ibada huleta matokeo chanya kwa anayeifanya.

Jambo la kutafakari na kujiuliza ni kwa nini tunaabudu lakini hatubadiliki? Kwa nini baadhi yetu tunaswali lakini hatujaweza kuacha dhambi ya uongo, zinaa na wizi? Kwa nini baadhi yetu kila mwaka tunafunga saumu ya mwezi Mtukufu wa Ramadhani lakini baada ya kumalizika mfungo jamii inarudi kulekule katika kutenda maovu na machafu? Kwa nini muumini amefanikiwa kutekeleza ibada ya Hijja lakini hajabadilika kitabia?.

Zipo sababu tano ambazo zinasababisha ibada yoyote isilete tija nazo ni: Moja, kufanya ibada bila ya kuwa na elimu ya ibada husika. Ieleweke kwamba ibada ni kazi inayohitaji elimu ya namna ya kuitekeleza.

Sasa ibada iliyokosewa kutokana na kukosa elimu kamwe haiwezi kuleta tija iliyotarajiwa. Ukweli ni kwamba mtu anapokosa elimu anaweza kufanya ibada kwa maana ya kushiriki ibada lakini katika uhalisia ibada husika hajaifanya.

Pili, kufanya ibada kwa kutumia mavazi, vyakula, vifaa vilivyopatikana kwa njia ya haramu. Unakuta mtu anaswali lakini amevaa nguo zilizopatikana kwa haramu, amekula chakula cha haramu na kadhalika.

Mtu wa aina hii hata akiswali kamwe hawezi kupata ile tija na baraka ya swala. Au unakuta mtu anafunga saumu ya mwezi mtukufu wa Ramadhani lakini daku alilokula ni la haramu au hata futari anayofuturu ni ya haramu. Kwa muktadha huo, tuelewe kwamba kuitumia haramu katika ibada kunaleta udhaifu katika ibada husika.

Tatu, kufanya ibada wakati fikra na moyo wote haupo pale kwenye ibada. Ibada yoyote ambayo yule anayeifanya, anaifanya kimwili lakini fikra na moyo wake haupo katika ibada hiyo haiwezi kukubaliwa na Mwenyezi Mungu, hivyo kamwe haiwezi kuleta tija inayokusudiwa.

Nne, kuzitekeleza ibada nje ya wakati au kuzitekeleza ibada baada ya kuchoka (kustaafu) na kwamba sasa hana kazi eti ndio anaona wakati wa kumuabudu Mwenyezi Mungu.

Swala inayoswaliwa nje ya wakati au swala zote za mchana zinakusanywa wakati wa Magharibi au Ishaa kisha zinaswaliwa kwa mpigo. Au swala zenyewe zinaswaliwa kama hakuna shughuli ikitokea kukiwa na shughuli ya maana swala inaachwa.

Ibada ya Hijja mtu anaamua kuitekeleza kwa kuwa sasa eti amestaafu na madhambi yote amepumzika. Utendaji ibada kwa mfumo huu hauwezi kuleta ile faida ya ibada.

Tano, kufanya ibada kwa kukidhi matakwa ya msimu au wakati sio kuabudu kwa lengo la kumuabudu na kumuogopa Mwenyezi Mungu. Unakuta mtu amefunga saumu lakini anatukana kama kawaida hana hofu hata chembe ya huyo Mola anaye muabudu.

Mtu amekwenda Umra au Hijja lakini huoni athari ya ibada katika uso wake na hana hofu hata moja ya huyo anayemuabudu.

Sababu hizi tukizichunguza na tukijichunguza tutagundua kwamba zimetuondolea 'ukali' wa ibada zetu. Tujirekebishe ili Mola wetu Muumba aturekebishie hali zetu na mambo yetu.

Wednesday, 3 January 2024

DHANA YA HIJRA KIISLAMU NA UELEWA WA MAKUNDI YA KIGAIDI



 

 

MAKALA katika ulimwengu huu kuna Imani za dini mbalimbali ambazo kila mmoja yupo huru kuamini imani yake kwa mujibu wa mafundisho ya dini anayoiamini. Hata hivyo kuna dhana mbalimbali ambazo baadhi waumini wanazitumia katika kufanya upotoshaji kwa faida na malengo yao.

Makala hii ya leo itaangazia miongoni mwa dhana ambazo zinazotumika kinyume na ukweli wake na kuchafuliwa na makundi mbalimbali yanayofanya matendo ya kihalifu yakiwemo makundi ya kigaidi, dhana hiyo ni ya "Hijra" ambayo imechukua nafasi kubwa katika Uislamu, ambapo inaashiria tukio la kihistoria la kutangaza mageuzi makubwa katika dini ya kiislamu na kuanza awamu mpya katika historia ya kiislamu.

Hijra iliyofanywa na Mtume Mohammed (S.A.W) ni tukio la kihistoria lililotenga enzi za kujificha na kuwalingania watu kwa siri na kufanyiwa matusi ya kila aina na kuanza enzi ya kutangaza dini na kuanzisha dola imara yenye nguzo yakujivunia na kuwa na nguvu ya kujitetea, pamoja na kupanua eneo la dola ili kuvutia umma kujiunga na dini hiyo mpaka dini yenyewe ikawa nguvu na imara.

Hijra katika sharia na historia ya kiislamu ni tukio la kihistoria la Mtume (S.A.W) ambalo ni muhimu kabisa wa waislamu wote ulimwenguni. Tukio hilo limeleta mabadiliko makubwa na likapelekea mabadiliko na maendeleo katika jamii ya waislamu ulimwenguni. Waislamu wanatakiwa kutafakari kwa umakini mafunzo ya tukio hilo na kuangalia taratibu alizozichukuwa Mtume (S.A.W.) na msimamo wa maswahaba wake watukufu (R.A.) kumuunga mkono na kumsaidia kwa ajili ya kufanikisha Hijra kwa mujibu wa maamrisho ya Mwenyezi Mungu (S.W).

Lile tukio la Hijra kimekusanya mafunzo mengi ambayo Makala moja au zaidi haitoshi kuyaelezea. Lakini tunayotaka kuyabainisha hapa ni baadhi tu kati ya mafunzo na mawaidha yaliyotolewa. La kusikitisha mno kuwa baadhi ya waislamu wakitumia mafunzo hayo kinyume na ilivyoelekezwa.

Kwa ujumla, Hijra ya Mtume (S.A.W.) japokuwa ilitokea Miaka 1440, lakini atakae tia amani na kukumbuka mazingira ya tukio na hilo na taratibu zake hatapata shida.

Ilihali, akiangalia na kuchambua historia hiyo, upata ufumbuzi na suluhisho kwa matatizo yake na changamoto zake zote. Kwahiyo tunaona kwamba kupanga na kujiandaa vizuri wakati wa kumtegemea Mwenyezi Mungu (S.W) na kumtii ndivyo msingi muhimu wa kumsaidia mtu kufikia malengo yake. Hilo ndilo funzo la kwanza tunalopaswa kulielewa.

Tukiangalia maana ya hadithi hii tunapata kufahamu hekima muhimu kabisa ndiyo kwamba muislamu japokuwa anatakiwa kumtegemea na kumtii Mwenyezi Mungu (S.W) lakini anatakiwa kujipanga na kutafakari vizuri ili aipate pepo njema. Lakini baadhi ya Makundi ya Kigaidi wamekuwa wakiitumia dhana ya "Hijra" katika tafsiri tofauti kwa lengo la kuwapotosha waislamu ambao hawakupata kuifahamu dini kwa undani zaidi.

Makundi ya kigaidi yamezoea kubadilisha dhana na kupotosha maana na kugeuza ukweli kuwa batili na lililoko sahihi liwe kosa na kinyume, kwa kutumia mbinu mbalimbali zinazokusudia kudanganya vijana na kuzishawishi akili zao. Kuhusu dhana ya "Hijra" makundi ya kigaidi yanadai kuwa hijra ni wajibu na faradhi juu ya kila muislamu na kwamba Hijra huwa kwa nchi ya kiislamu ambayo kwa mtizamo wao ni ile nchi inayodhibitiwa na wao wakishikilia kauli yake Mtume (S.A.W.) "Hakika Hijra haitakatika endapo makafiri wanapiganiwa" na kauli yake (S.A.W.) iliyopokelewa na Mua'wiya anasema "Hakika Hijra haitakatika mpaka taiba ikatike na taiba haitakatika mpaka jua likuche kutoka upande wa magharibi".

Pia wenye fikra hizo wanatumia Qur'an kwa kuunga mkono mtizamo huo, ambapo wanadhani kuwa agizo la Mwenyezi Mungu (S.W.) kwa waja wake kuhama ni kwa jumla na linajumuisha hali zote kwa mujibu wa kauli ya Mwenye Mungu (S.W.).

Aya nyingine inayotumika na makundi ya kigaidi kupotosha watu wasiyokuwa na elimu ya dini ili kuthibitisha uwajibu wa Hijra ni kauli ya Mwenyezi Mungu (S.W.) "na mwenye kuhama katika njia ya Mwenyezi Mungu atapata pengi duniani pa kukimbilia, na hatapata wasaa. Na anayetoka nyumbani kwake kuhama kwa ajili ya mwenyezi Mungu na Mtume wake, kasha yakamfika mauti njiani basi umethibiti ujira wake kwa Mwenyezi mungu na Mwenyezi Mungu ndiye mwenye kurehemu" (Al - Nisaa: 100).

Kimsingi makundi ya kigaidi yamekuwa yakitumia yakifanya upotoshaji kutumia Aya hizo, pasipo imani na utulivu wa akili na kama hukupata elimu ya dini vizuri, vijana wengi wamekuwa wakirubuniwa kwenda Hijra pasipo kujuwa kuwa wanakwenda kutumika kutekeleza malengo ya kisiasa na kihalifu kwa vikundi vya kigaidi.

Dhana ya Hijra ina maana na matumizi tofauti na uelewa wa makundi ya kigaidi na kwamba makusudi ya Hijra katika sharia za kiislamu ni kuhama kwa ajili ya kuinusuru dini na kujilinda kutokana na fitina kutoka ardhi isiyofaa kwenda ardhi au nchi yenye amani na utulivu na kuwezesha mtu kukimu maisha yake katika mazingira mazuri na si kutafuta dola ya kiislamu na kuuwa watu wasiokuwa na hatia.

Friday, 29 December 2023

ZIFAHAMU BAADHI YA AYA ZA QURAAN ZINAZOHIMIZA AMANI NA MATENDO MEMA KWA BINADAMU WOTE

 



Ndugu wasomaji wangu karibuni katika Makala yetu ya leo ikielezea baadhi ya aya zinazohimiza amani na upendo. Katika Uislamu, Quraan ni maandiko matakatifu ambayo yanatoa mafundisho kwa waumini wa dini hiyo, katika maandiko hayo kuna baadhi ya aya ambazo zinatumika katika kusisitiza matendo ya amani kama ilivyo maana ya neno 'islamu', ambapo matendo hayo yanapelekea binadamu kuwa na mwisho mwema hapa duniani na akhera.

Vile vile uwepo kwa matendo hayo mema yanayopelekea kuwepo kwa amani na utulivu yatasaidia jamii kupata maendeleo.

Ili kuishi katika matendo hayo mema ni vyema kujifunza elimu ya dini ikiwemo Qur,ani, hadithi na sunna za mtume Muhammad (S.A.W).

Zifuatazo ni baadhi ya aya ambazo zinahimiza amani na matendo ya Amani katika dini ya kiislamu.

AYAYA8 katika SURAT MAIDAH, Aya hii inaeleza kuwa "Enyi waumini simameni imara kwaajili ya Mwenyezi Mungu na mchukue haki ushuhuda. Usiruhusu chuki ya watu ikupeleke kwenye dhulma. Kuwa mwadilifu, huko ndiko karibu na haki. Na mcheni Mwenyezi Mungu Hakika Mwenyezi Mungu anayo habari za mnayotenda". Lengo kuu la mafundisho ya aya hii ni kutenda haki na kutomtendea mtu mwengine mabaya bila kujali dini yake, kabila hata rangi.

Katika SURAT QAAF AYA 45, Aya hii imeeleza kuwa "Sisi tunajua Zaidi wanachosema na wewe Ewe Mtume si wakuwalazimisha kuamini, hivyo wakumbushe kwa quraan tu sio kuwalazimisha", lengo la aya hii kuhimiza matumizi sahihi ya quraani hasa katika kuwalingania watu na kutumia nguvu na vitisho kama wanavyofanya wanaharakati. Aya hii ikufuatwa ipasavyo itasaidia kuwepo kwa matendo ya amani ana utulivu katika jamii.

AYA YA 14 katika SURAT JATHIYAH, Aya hii imeeleza kuwa "Sema, Ewe Muhammed, kwa wale walioamini kwamba wawasamehe wale wasiotarajia siku za Mwenyezi Mungu, ili awalipe watu kwa yale waliyokuwa wakiyachuma " lengo la aya hii ni kuwa kwa mtu anayekosea haukumiwi na binaadamu mwenzie bali Mungu ndio anayetoa hukumu na endapo akatokea mtu au kikundi cha watu akahukumu watu wengine atakuwa ameenda kinyume na maamrishio ya Mwenyezi Mungu na Mtume Muhhammed (S.A.W)

Katika SURAT BAQARA AYA AYA 194, Aya hii imeeleza kuwa "kutakuwa na kisasi katika mwezi mtakatifu kwa kosa katika mwezi mtakatifu na ukiukwaji wote utaleta kisasi. Kwa hiyo, mtu akikushambulia, lipiza vivyo hivyo lakini kumbuka Mwenyezi Mungu na jueni kwamba Mwenyezi Mungu yupo pamoja na wacha Mungu". Lengo la aya hii ni kuwa kazi ya kuhukumu aachiwe Mwenyezi Mungu, badala ya hukumu hiyo kufanywa na binaadamu dhidi ya binaadamu wenzao.

AYA 161 katika SURAT AL ANAFAL, Aya hii imeeleza kuwa "ikiwa adui ana mwelekeo wa amani, fanya amani nao. Na mtegemee Mwenyezi Mungu .Hakika yeye peke yake ndio mwenye kusikia, mjuzi wa yote " lengo la aya hii ni kusisitiza amani na utulivu miongoni mwa binaadamu wote na hukumu mwenye haki ya kutoa ni Mungu pekee.

Wito wangu kuwa elimu ni (mali, bahari, rasilimali, ufunguo wa maisha, ukombozi, uhai na fumbo la ujinga), hivyo kuna umuhimu mkubwa kwa jamii kupata elimu ili kujikomboa kifikra na kuzuia watu wasiingie katika vitendo viovu katika jamii ambavyo vinaweza kuleta athari kubwa katika jamii.

Hata hivyo kuna umuhimu wa kusoma elimu (elimu ya dini) ili kupata maana sahihi za aya mbalimbali hasa zinazohimiza kuwepo kwa amani na utulivu, hali hilo itasaidia kuwepo kwa maendeleo katika jamii na Nchi kwa ujumla. Pia ufahamu wa aya hizo utasaidia kubaini watu ambao wanataka kutumia aya hizo kufanya upotoshaji kwa wengine.

Monday, 18 December 2023

MSAMAHA NA DHANA ZAKE


Ndugu wasomaji karibuni katika Makala yetu ya leo ambayo inahusu jambo muhimu na msingi wa uwepo wa amani na utulivu katika maisha yetu ya kila siku. Mada hii ya msamaha ni muhimu kwa sababu inahusisha hisia za mtu moja kwa moja katika kufanya maamuzi baada ya kukosewa au kukosea.

Neno Msamaha linatafsiriwa kwa dhana mbalimbali kama ni uamuzi wa Mwenyezi Mungu au mtu mwingine wa kuamua kutofuatilia matendo na makosa ambayo ametendewa na mtu mwingine.

Katika Luka 6:37 imeelezwa kuwa maana ya msamaha ni "kuachilia". achilieni nanyi mtaachiliwa.

Katika Quraani Surat taghabun aya ya 14 imeeleza maana ya neno msamaha na hatua zake ambapo imefafanuliwa kuwa msamaha au kuwia radhi ni hali ya kutotilia mkazo au maanani kosa lililofanyika hii kwa mujibu wa Imamu Ali (A). Msamaha ni taji la sifa kwa muungwana. Pia katika aya hii imeeleza kuwa msamaha ni uvumilivu ambao unazuia kuadhibu kwa maneno au vitendo, kadhalika msamaha ni kufuta kile kitendo kilichofanywa na kuondoa dhana ya matokeo hasi ambayo yametokana na kufanyiwa makosa.

Vile vile tafsiri hii ya neno msamaha inazidi kueleza kuwa ni kinyume kabisa cha neno kisasi lakini ni tofauti na neno kusahau, kutetea au kupatana na aliyekiri makosa. Hii ina maana kuwa mtu anaweza akakusamehe ila bado akawa hajasahau lile jambo au tukio alilotendewa na mtu aliyemkosea.

Kwa upande wa dini zote unasisitiza na kuhimiza watu kusamehe pindi wanapokosewa, hali hiyo ya kusamehe inaleta nguvu hasa kwa mtu anayetoa msamaha na nafuu hiyo inaweza kuenea kuanzia katika nafsi ya mtoaji msamaha na mwili wake mzima.

Msamaha siku zote unajumuisha mambo matatu ambayo ni msamaha wenyewe, uvumilivu na kuachiliwa.

Chanzo kikuu cha msamaha kilianza pale dhambi na makosa yalipoanza maana pasipo na dhambi na makosa msamaha usingekuwepo. Hivyo msamaha upo maalumu kwa ajili ya wale binadamu ambao ni watenda dhambi na wafanya makosa.

Kwahiyo, tambua kwenye dhambi na makosa hapo ndipo penye msamaha. Kuomba msamaha ni roho na mtu ambaye atagoma kuomba msamaha basi huyo ana roho ya kishetani maana naye aligoma kuomba msamaha pindi alipomkosea Mwenyezi Mungu na Shetani kuahidi kuwa atawapoteza na waja wengine.

Ili uwe mtu mwenye uwezo wa kutoa msamaha dhidi ya aliyekukosea lazima uwe na sifa zifuatazo.

Uwe mtu mwenye huruma, mtu mwenye uvumilivu, mtu mwenye upendo dhidi ya watu wengine, lazima uwe mtu uliye na hofu ya Mwenyezi Mungu pamoja na kumjua vyema Mwenyezi Mungu na kwamba Mungu yeye ndiye aliyeanzisha msamaha kwa wanaomkosea mwisho mtu mwenye uwezo wa kutoa msamaha huwa ambaye anajua umuhimu wa msamaha pindi anapokosewa.

Je, utatambuaje au dalili na ishara za mtu aliyekusamehe baada ya kumkosea.

Hawezi kukuzungumzia vibaya mbele ya watu wengine, atakuchangamkia tena kama ilivyokuwa kabla ya kukoseana, endapo utapatwa au utakuwa na shida au tatizo hatosita kukusaidia na atakusaidia bila kinyongo chochote, pia mtu aliyekusamehe atakuwa anakusalimia na kupokea salamu zako pindi unapomsalimia kama ilivyokuwa zamani.

Vile vile katika tendo zima la msamaha mtu anayekusamehe anaweza kufanya hivyo bila kumuomba msamaha ila kama itatakiwa aliyekosea mpaka aombe msamaha yeye kuna mambo muhimu ya kuzingatia ambayo ni:-

Afahamu na kujua njia sahihi ya kuomba msamaha ikiwa hata kulia au kupiga magoti ili amridhishe anayemuomba msamaha, mwombaji msamaha afahamu faida na umuhimu wa kuomba msamaha juu ya lile kosa alilotenda, ajue namna nzuri ya kuacha kutorudia kosa alilotenda awali, mwisho na muhimu zaidi awe na imani kuwa Mwenyezi Mungu amehimiza kuomba msamaha pale tunapokoseana.

Wito wangu ni kuwa makosa kwa maumbile ya mwanadamu ni jambo la kawaida ingawa anaweza kukosea bahati mbaya ama makusudi. Hata hivyo kwa hali yoyote ile bado haizuii kwa mtu aliyekosea kusamehewa kwa kosa alilotenda. Siku zote msamaha huleta furaha na amani ya moyo hii itasaidia kupata jamii na Taifa lenye upendo, utulivu na amani ambapo itasukuma uwepo wa maendeleo kwa vizazi husika.
 

Tuesday, 12 December 2023

FAIDA YA KUDHIBITI HASIRA

 


 

Wapendwa wasomaji wangu, karibuni katika Makala yetu ya leo ikizungumzia mada ya hasira Hasira ni hali inayompata binadamu au mnyama mbele ya kipingamizi na katika hali hiyo mtu hughadhibika, hukwazika, kuchukia na hata kupata kitu ambacho yeye muhusika hapendi kuwa nacho.

Madhara ya uwepo kwa hasira hasa ya mara kwa mara inaweza kusababisha kuwepo kwa matendo maovu na ya kikatili ikiwemo mauaji, uharibifu wa mali ambayo yatakuwa na athari kwake, jamii na Taifa kwa ujumla.

Ili kuepuka kadhia hiyo kuna njia sahihi ya kukwepa hasira kwa mtu inayompata mara kwa mara hivyo mara nyingi anashauriwa ajaribu kuepuka vitu au mambo yanayoweza kumpelekea kumuudhi kwa mfano kuepuka kujibizana itamsaidia kuepuka ugomvi dhidi ya watu wengine.

Pia ni vyema kuepuka kuendelea kumuudhi mtu mwingine pale unapoona kuwa jambo au kitu unachomfanyia kinamkwaza maana kitendo cha kuendelea kufanya hivyo kinaweza kusababisha kutokea kwa athari na madhara makubwa.

Siku zote kitendo cha kutodhibiti hasira ni kwenda kinyume na maamrisho ya Mwenyezi Mungu kwa dini zote sababu amehimiza kuepuka hasira maana matendo yatokanayo na hasira husababisha ukatili na uovu mkubwa kwa jamii na Taifa kwa ujumla, vilevile hasira husababisha matatizo makubwa ya milele hapa duniani na akhera.

Kisayansi kudhibiti hasira ni muhimu kwa sababu kunasaidia kuepuka athari zifuatazo ambapo mtu mwenye hasira inampelekea kupunguza uwezo wa kufikiria kutokana na ubongo kuathirika hivyo hupoteza kumbukumbu na kupelekea kufanya matendo mabaya, hasira inaweza kusababisha kupata tatizo la moyo, vidonda vya tumbo, vile vile hasira inasababisha tatizo la kupungua kwa kinga ya mwili.

 

Kwa upande wa mwanamke inasababisha kuvurugika kwa mzunguko wa hedhi sababu kuu ni kutokea kwa mabadiliko ya mzunguko wa homoni na hata wakati mwengine hasira kupelekea kuharibika kwa ujauzito.

Ili kuepuka kuwa na hasira inatakiwa yafanyike mambo yafuatayo. Kwanza kujua sababu ya kuwa na hasira zako kwa maana ya nini kinapelekea, pili kujua na kukwepa sababu za hasira ulizonazo, tatu kujizuia kuchukua hatua na kufanya jambo lolote baya pale unapopatwa na hasira, wakati mwingine kitaalamu unashauriwa uhesabu hadi ishirini ili ujipe muda wa kuchukua maamuzi yako yanayotokana na hasira uliyonayo na kama kuhesabu anzia 20 kwenda 1.

Vile vile ili kumaliza hasira jitahidi kufanya kitu au jambo lingine mbadala, jitahidi kukaa kimya ili kuzuia kuongezeka kwa hasira, ondoka eneo au mazingira ambayo yamekupelekea au kusababisha hasira, badili mada na aina ya mazungumzo pamoja na mtu ambaye amekusababishia upate hasira. Jambo la kuzingatia ni kuwa suala la kuwa na hasira halishabihiani na hali mtu, uwezo wake, elimu yake, dini, kabila, rangi, umri, jinsi na hata cheo chake.

Hivyo ni muhimu kwa kila mmoja kuhakikisha kuwa anaheshimu mipaka ya ubinadamu na utu kwa mwengine ili kuzuia kusababisha kutokea kwa sababu ya kupata hasira. Waswahili wanasema heri lawama kuliko fedheha wakimaanisha ni bora ukakubali kujishusha na kuwa mpole ili kuepuka kusababisha hasira kuliko kutaka kujibizana ambapo hali itapelekea kushikwa kwa hasira na kufanya maamuzi ya hatari yenye hasara kwako, jamii na Taifa kwa ujumla kwa maana nyingine ni kuwa (hasira hasara).

Wito wangu ni vyema kila mmoja kuhakikisha anadhibiti hasira zake pindi anapopatwa na jambo au kitu kinachomkwaza au kumuudhi, katika hatua hii kuna baadhi ya watu wenye mlengo wa kupotosha watu wengine wanaweza pia kutumia maneno au kufanya vitendo vya uchonganishi dhidi ya dini nyingine, Serikali au jamii nyingine ili kuwakwaza na kuwaudhi wengine kwa lengo la kuwasababishia hasira itakayowapelekea kufanya vitendo vya kihalifu dhidi ya makundi hayo wanayochonganishwa nayo.

Hivyo ni muhimu kwa kila mmoja kusoma alama za nyakati ili kuweza kubaini lengo la mtu anayekusababishia hasira, kufanya hivyo itasaidia kuwa na uwezo wa kukwepa sababu za kupata hasira. Tuendelee kudhibiti hasira zetu ili kuendelea kulinda amani na utulivu katika jamii na Nchi kwa ujumla.

MSAMAHA NA DHANA ZAKE

    Ndugu wasomaji karibuni katika Makala yetu ya leo ambayo inahusu jambo muhimu na msingi wa uwepo wa amani na utulivu katika maisha yetu...